Umezungukwa na watu wa aina gani?

Habari za muda huu ndugu msomaji wa mtandao huu wa PAMBAZUKA DAIMA. Ni matumaini yangu kwamba unaendelea kusonga mbele licha ya changamoto za hapa na pale unazokutana nazo, changamoto hizo ni magurudumu katika safari yako. Kwa wale waliokuwa wananifuatilia hapo zamani watakumbuka kuwa nilikuwa naandika kupitia blog ya Life Adventures ambayo nimehamishia makala zote huku na kwa wasomaji wapya nitumie fursa hii kuwakaribisha.

Ndugu msomaji katika hii dunia tumezungukwa na vitu mbalimbali. Tumezungukwa na watu, vitu, mimea na hata wanyama. Vitu hivi vyote vinaweza kutuathiri kwa namna hasi au namna chanya. Tunaweza kuathiriwa zaidi na binadamu wenzetu kuliko tunavyoweza kuathiriwa na vitu vingine. Lakini pia sio kila binadamu anaweza kutuathiri bali wale ambao tunatumia muda wetu mwingi nao. Hao si wengine bali ni ndugu,jamaa na marafiki. Ndio, hao ndio watu ambao mara nyingi tunapendezwa nao na hivyo kujikuta kwamba tuko nao muda mwingi sana kiasi cha kuweza kutuathiri. Kuna msemo wa Kiswahili usemao kwamba unaweza kuchagua marafiki lakini huwezi kuchagua ndugu na majirani. Huu msemo uko sawa kabisa kwani kama ndugu zako si watu wazuri huwezi kuwakataa kuwa si ndugu zako, vile vile unaweza kuwa na majirani wabaya sehemu unayoishi sasa ama ukajikuta kwamba kila unapohamia unakutana na watu wa ajabu tu. Sote tuna uwezo mmoja mkubwa wa kuchagua marafiki, ndio marafiki tunaoona tunaendana nao, marafiki ambao tabia zao zitatujenga kuliko kutubomoa. Labda sisi tuliopo katika kizazi hiki cha teknolojia tuna nafasi kubwa ya kuathiriwa hata na watu tusiowafahamu kuliko vizazi vilivyotutangulia hasa kupitia mitandao ya kijamii kama facebook, whatsapp, telegram, tweeter,instagram nk. Tunaweza kujaza hisia hasi ama chanya kwa haraka zaidi kuliko kipindi chochote kingine katika historia ya dunia hii. Bahati mbaya ni kwamba wengi wamekuwa wakitumia mitandao hii kwa kubomoa zaidi kuliko kujenga. Ni muda sasa wa wewe kutafakari aina ya makundi ya kijamii ama watu waliopo mitandaoni unaowafuatilia. Usikae katika kundi au mtandao wa kijamii usiokujenga,bali kaa sehemu ambayo unaweza kuambukizwa chaji chanya za maisha.

Tabia za watu wengine huathiriwa zaidi na tabia za marafiki zao au watu anaotumia nao muda wake mwingi. Kama utakuwa na marfiki walevi bila shaka nawe utakuwa mlevi, ukiwa na marfiki wezi nawe utakuwa vile vile, ukiwa na marafiki wenye mafanikio nawe pia utakuwa na mafanikio na hata pia ukiwa na marafiki walalamikaji nawe utakuwa mlalamikaji vile vile. Unaweza kupingana nami lakini ukweli ni kwamba ndege wafananao huruka pamoja.Mafanikio yetu ni wastani wa watu wa tano tunatumia muda wetu mwingi na wao. Mbuzi hawezi kukaa na mnyama mwingine muda mrefu kama afanyavyo kwa mbuzi mwenyewe. Tabia za watu walikuzunguka zinaakisi tabia zako. Kama watu hawana uhakika na tabia zako basi wataangalia tabia za marafiki zako, hii ni kwa sababu mtu huvutiwa na tabia za wanaomzunguka. Ndugu, jamaa na marafiki wana nafasi kubwa sana ya kutuathiri na kutufanya tufanikiwe ama tusifanikiwe katika kile tunachokifanya. Kama una marafiki wakatishaji tamaa nawe utakuwa mkatishaji tamaa ama mkata tamaa mwenyewe. Marafiki hasi na walalamikaji watakufanya kuwa mmoja wao na sio tofauti nao, marafiki waoga huwa na marafiki waoga ama ambao wataambukizwa tabia hizo za uoga.

Ni muda sasa wa kutathmini aina ya watu wanaokuzunguka kama ni watu wanaokusaidia kusonga mbele ama kurudi nyuma. Kama ni kundi la kukupeleka mbele basi unaweza kuendelea nao na kama ni wa kukurudisha nyuma,acha kutumia muda wako mwingi na wao. Sijasema uwatenge la hasha ila kupunguza ukaribu nao na utafute marafiki wenye malengo sawa na yako, marafiki chanya na marafiki wenye msaada kwako kwa namna moja au nyingine. Kama ni ndugu najua kabisa huwezi kuwakataa kwamba sio ndugu zako bali cha kufanya ni kutokaa nao muda mrefu kiasi cha kukuathiri, unaweza kutumia muda mfupi tu kujuliana hali ama kujadili masuala muhimu ya familia pale inapobidi. Tafuta watu werevu kama wewe au kuliko wewe, ambao unaweza kujifunza kutoka kwao. Kuna mtu aliwahi kusema kwamba kama katika kundi wewe ndiye mtu mwerevu pekee basi ni muda wa kuliacha hilo kundi na kutafuta kundi lingine. Hii ni kwa sababu badala yaw ewe kujifunza kutoka kwao utaweteka na kujisahahu ama kujiona wewe ndio kila kitu na kubweteka na huku pia jamaa hao wakikunyonya badala ya kusaidiana. Usiogope kuwapoteza marafki ambao wanakuvuta kuelekea nyuma, marafiki waliojaa mawazo hasi au marafiki wanaokunyonya,siku zote kuwa na watu mtakaofaidishana (win-win situation). Utapata marafiki wengine bora zaidi.

Kumbuka kwamba marafiki na watu walikuzunguka wana nafasi kubwa ya kuamua kiasi cha mafanikio yako, ni lazima uchukue hatua mara moja kabla hujachelewa. Tafuta watu chanya, watu wenye kukusongesha mbele, watu wenye kutia moyo na watu wenye kukusaidia pale unapohitaji msaada wao au watakapoona unahitaji msaada. Kuna marafiki wanawaza kukata tamaa muda wote, wegine wanawaza starehe muda mwingi na wengine wanawaza kuhusu namna ya kufanya makubwa. Ni heri uwe peke yako kuliko kuwa na marafiki hasi. Kubali ukatae ukikaa na kundi lolote nililotaja utaanza kuzoea (adapt) hali hiyo na kuona ni kawaida. Unadhani watu wengi wameanza kunywa pombe, kuvuta bangi na sigara, ujambazi na tabia zinazofanana na hizo kupitia nani kama sio ndugu, jamaa na kwa kiasi kikubwa sana marafiki? Ni vigumu kukutwa kwenye kundi la majambazi halafu watu wakaamini kwamba wewe sio jambazi.

Marafiki wawe chachu ya wewe kusonga mbele na sio kukurudisha nyuma. Watu waliofanikiwa hukaa na watu waliofanikiwa. Watu wasiofanikiwa hukaa na watu wasiofanikiwa, hawachangamani kama ilivyo kwa mafuta na maji. Kuna msemo wa KIkemia usemao ‘’Like dissolve like’’ ukiwa na maana kwamba vitu vinavyofanana huyeyushana kwa vyenyewe mfano maji kwa maji na mafuta kwa mafuta. Hivyo hata kama hukuwa na tabia fulani utaambukizwa kutoka kwa marafiki zako. Kulikuwa na jamaa ambae kila mwaka mpya wa masomo ukianza alipokuwa anasoma alikuwa akiwaambia watu kuwa baadhi ya masomo ni magumu sana na uanaweza kufeli, ama mwalimu fulani ni mbaya. Unajua kilichotokea? Ni kwamba maneno yake ya kukatisha tamaa na ya kujirudiarudia yaliwaingia baadhi ya watu moyoni na kwenye akili na kutengeneza ugumu wa masomo husika ambayo hatima yake ni kwamba walifeli masomo husika. Ugumu aliouona yeye aliwaambukiza marafiki zake. Sio tu kwamba aliwaambukiza tabia hiyo bali pia tabia zingine ambazo pengine zisingefaa kwenye jamii iliyostaarabika. Kila mtu ana rafiki, ndugu au jamaa ambae amemgusa kwa namna moja ama nyingine iwe hasi au chanya. Kila mtu anaweza kutoa mfano wa rafiki yake mwenye tabia fulani kama akipewa nafasi. Ni muda wa kukaa mbali na rafiki mwenye tabia kama nilizotaja kwenye mfano ama ubaki nae uangamie.

Kama kuna mtu ambae alikuwa masikini na kushinda maskani ama kijiweni, siku akianza kufanikwa hupata marafiki wenye mafanikio ama alihama kuwatafuta watu wenye mafanikio wenzake. Ni vigumu sana kuwakuta matajiri katika vijiwe vya masikini na hii hupelekea masikini au watu uliokuwa nao kijiweni kusema kwamba umeanza kuringa baada ya kuanza kutajirika, unakumbuka ‘’like dissolve like?’’. Siku alifanikiwa akianza kurudi kijiweni kukaa na wale watu wenye mawazo hasi, kuna mawili yanweza kutokea nayo ni yeye kuwapandisha kwa kuwabadili ( na inaweza kuwa ngumu pia) ama yeye kurudishwa nyuma ili aweze kufanana nao. Badili marafiki kabla hajakubadili wewe,badili maisha yako.

Wajali ndugu,jamaa na marafiki zako kwa kuwatumia makala hii. Pia usisahau kujiunga nasi kwa email ili kupata makala na vitabu na kuLike page yetu Facebook kwa kunyeza hapa. Kupata makala za Afya,Chakula na Lishe bonye za Hapa
Nickson Yohanes

nmyohanes@gmail.com

Utofauti mmoja mkubwa uliopo baina ya mfugaji na mvuvi

Hbari mpendwa msomaji wa mtandao huu wa PAMBAZUKA DAIMA ni matumaini yangu kwamba unazidi kulisongesha gurudumu la kuelekea kwenye mafanikio ya maisha yako.

Leo ningependa nikushirishe kuhusu utofauti mmoja uliopo kati ya mfugaji na muwindaji au mvuvi.
Sote tunajua kuwa jamii zote hizi nilizojata zinategemea wanyama kwaajili ya kuendesha  maisha yao, wafugaji wakiwategemea wanyama wawafuagao huku wavuvi wakitegemea kuendesha maisha yao kwa kuvua samaki na wawindaji wao wakitegemea kuwinda wanyama wa porini kuendesha maisha yao. Japo jamii za uwindaji zinaonekana kama zimekwisha katika karne hii bado kuna jamii chache sana zinazotegemea kuishi kwa kutegemea uwindaji.

Mfugaji ni yule mtu anaefanya kazi ya kuwatunza wanyama na kuwafanya waongezeke maradufu. Huwawekea mazingira mazuri ya kuishi, matibabu na malisho. Huishi kwa kuwategemea kwa chakula hasa maziwa na nyama. Muwindaji hachinji wanyama wake ovyo bali huwachinja kwa utaratibu maalum tena baada ya kuongezeka sana. Umeshawahi kumuona mfugaji mwenye ng’ombe mmoja akaamua kumchinja? Jibu ni hapana. Kitu kingine ni kwamba wafugaji wengi huwapenda sana mifugo yao kiasi kwamba hawawachinji au kuwauza mara kwa mara. Ni kutokana na tabia hii ya wafugaji kujikuta wana mifugo wengi. Mifugo ninayoizungumza ni ile mifugo ya kawaida ambayo hata Tanzania tunao kama ng’ombe, mbuzi, kondoo, kuku na hata samaki. Hivyo basi tabia ya mfugaji tunayoiona hapa ni kusubiri kula mazao yatokanayo na mifugo yake na sio kula mifugo yake kabla haijazaliana.



Kwa upande wa muwindaji au mvuvi yeye anaamini kwamba pori, ziwa, mto au bahari zipo tu na samaki wataendelea kuwepo. Si ajabu kukuta mvuvi au muwindaji kutokuwa na akiba yoyote ya kumtosha kwa siku kadhaa, si bahari, mto au ziwa lipo bhana?sasa kwanini ahangaike, hamna sababu (kwa mawazo yake). Tatizo ni pale ambapo atakosa uwezo wa kuvua ama kwa uzee au ugonjwa, lazima familia itatereka kwa kukosa mahitaji muhimu. Pia kuna kipindi serikali hufunga mito, mabwawa na maziwa ili kuruhusu samaki kuzaliana. Wakati huo huo aliefuga samaki anaweza kuendelea kuishi.
Maisha ya muwindaji na mvuvi ni ya kula na kutumia kile chochote anachokipata, hakuna akiba na wala hakuna kesho. Mfugaji yeye ana akiba ya mifugo yake na huitumia pale ambapo anapata tatizo. Muwindaji hawezi kwenda porini kuchukua wanyama walio hai ili kuwatunza, hana muda wala uvumilivu huo. Muwindaji na mvuvi hawaweki akiba ya walichokipata ama kukiendeleza ili kiwe kikubwa ili kesho kiwasaidie, hawafikiri katika kuzalisha bali kutumia tu. Hawa watu wanakula kila kitu na kusahau kukuza ili kesho kiwape faida. Wanasahau kuwa akiba haiozi.


Mpendwa msomaji mfano wa mfugaji na mvuvi ni mfano uliopo katika jamii zetu.Inawezekana kabisa wewe una tabia zote za mfugaji au una tabia zote za mvuvi/mwindaji. Ni muda sasa wa kujifanyia tathmini. Kuna wale ambao huweka akiba na kukuza vipato vyao ili viwasaidie baadae na hao ndio mfano wa mfugaji na kuna wale ambao hutafuna kila kitu walichojaaliwa kukipata,hawa ndio wavuvi. Bila shaka wewe unajijua upo kundi gani, kundi la mfugaji au kundi la mvuvi. Ni mara nyingi sana unakuta mtu anapata kipato na kuamua kutumia chote hasa mshahara akijua kwamba mwisho wa mwezi ataupata mwingine,huyu hana tofauti na mvuvi mwenye imani na bahari bila kujali kwamba kuna mawimbi, bila kujali kwamba kuna kukauka kwa mito na kupungua kwa kina cha maziwa na samaki kuzaliana. Watu hawa mwisho wa mwezi unaweza kuwakuta wakiwa hawana kitu na kuanza kuishi kwa kukopa. Yeye akipata hela hutumia katika kununua vitu ambavyo haviwezi kumzalishia mali. Mtu huyu ambae ni mvuvi hatakuwa na uwezo wa kusonga mbele hata siku moja. Ataanzaje kwa mfano wakati hana mnyama ambae kesho atazaa na kuwa nao wawili au watatu? Kama unataka kusonga mbele na kufanikisha malengo yako ni muhimu uache kuwa mvuvi na kuamua kufuga, ni muhimu kuana kujiwekea akiba. Kuna msemo wa kiingereza usemao ‘’A dollar saved is a dollar earned’’ ukiwa na maana kwamba ‘’Dola moja iliyowekwa akiba ni dola iliyokwishwa kupatikana’’. 

Katika kitabu kitakatifu cha biblia, kuna mfano wa pacha wawili, mkubwa akiitwa Essau na mdogo akiitwa Yakobo. Essau alikuwa ni mwindaji na Yakobo alikuwa mfugaji. Siku ambayo baba yao alitaka kumbariki Essau alimtuma akawinde amletee nyama aweze kumbariki. Mdogo mtu na mamaye waliamua kumchukua mnyama ambae anafugwa na kumuandaa kisha kumpelekea baba yao Isaka. Mpaka muda huo Essau alikuwa ameshachelewa na hivyo kukosa baraka kutoka kwa baba yake. Laiti kama Esau angelikuwa na wanyama pale nyumbani pengine asingechelewa kupata baraka alizopanga kutoa baba yake kwake. Akiba aliyokuwa nayo Yakobo ilimfanya awahi fursa ya baraka. Ni mara ngapi umezikosa fursa muhimu kwa sababu ya kutokuwa na akiba? Unapokula kumbuka kuna kesho pia.
SOMA: Je mtaji ni kikwazo kwako katika kuanza biashara au kuwekeza?

 Kama utaamua kujiwekea akiba mathalani ya pesa ni muhimu sana kuifanya iendelee  kukua kwa kuizungusha ili iweze kuzalisha nyingine. Mwadishi mmoja aliwahi kusumea kwamba hela isiyozungushwa ni sawa na gazeti la zamani. Gazeti la leo halitakuwa na thamani kesho ama kesho kutwa,matumizi yake ni leo tu. Huwezi kwenda kwa muuza magazeti kununua gazeti la mwezi uliopita, kwanza ni vigumu kulipata. Akiba utakayoipata iwekeze ili kipato chako kizidi kukua. Kila mara jiulize kama wewe ni mfugaji au mvuvi. Acha kununua vitu ambavyo havikuzalishii chochote na uanze kununua vitu vitakavyoongeza kipato chako. Watu ambao tayari ni matajiri na wale wenye akili na mawazo ya kitajiri hawanunui vitu vya anasa kwa kipato au mtaji wao bali kwa faida waipatayo kupitia vyanzo walivyovianzisha. Kwanini umchinje ng’ombe mmoja ulienae kwaajili ya sherehe badala ya kusubiri umchinje ndama wake? Kwa nini ufurahie kwa muda muda mfupi na kuteseka kwa muda wote uliobakia? Kubali kuahirisha mambo yenye kusubiri kwa mambo yasiyoweza kusubiri.

Pia katika mfano wa mfugaji na mvuvi tunona tabia nyingine ya mvuvi ni kutokuwa na subira wala uvumilivu, yeye anachojali ni kutuliza njaa yake ya leo. Wakati mfugaji anavumilia dhoruba zitokanazo na mifugo yake. Anajua kuna magonjwa, njaa nk. Maana yake tunahitaji uvumilivu ili kuweza kukua, huwezi kuzaliwa leo na kutembea kesho. Lazima usubiri. Usione kwamba unapitwa, simamia katika malengo yako na usubiri huku ukiendelea kuboresha mbinu zako za kongeza kipato. Usiogope kuanza na kitu kidogo na kukua kuliko kusubiri mpaka kiwe kikubwa ndipo uanze, ukweli ni kwamba hiyo siku haitakaa ifike. Mfugaji anaweza kuanza na kuku au ng’ombe wawili na baada ya muda fulani akawa nao wengi wakati huo mwingine akisubri apate pesa za kuanza na mia. 

Nakushauri uwe na tabia za mfugaji kuweka akiba kisha kuwekeza katika vitu vyenye kuzalisha. Haiwezekani una vutu vyenye thamani kubwa ndani halafu huna uhakika wa kuishi ikitokea umefukuzwa au kusimamishwa kazi. Maisha ya ajira hayatabiriki hivyo anza kujiwekea akiba na kutafuta kitu cha kufanya. Vitu vyote vizuri utavinunua kwa faida na sio kwa mtaji. Matajiri unawaona walijinyima vitu vya thamani au anasa kwanza ili waweze kutengeneza mifereji ya utajiri.

Nina imani kuwa umenufaika na makala hii. Wasambazie wale uwapendao.

Pia usisahau kupenda ukurasa wetu wa facebook kwa kubonyeza hapa na kujiunga na orodha yetu ya email kwa makala nzuri kila mara. Kwa makala za Afya na Lishe bonyeza hapa

Nickson Yohanes
nmyohanes@gmail.com


Hii ndiyo siri ya kuweza kupokea au kupata kitu chochote

Habari za leo ndugu msomaji wa mtandao huu wa PAMBAZUKA DAIMA ni matumaini yangu kwamba bado unaendelea kulisukuma gurudumu la maendeleo kwa kufanya kitu bora zaidi ya ulivyofanya jana.

Ndugu msomaji kuna siri katika kila kitu ambacho ukifanikiwa kuijua basi utaweza kufanikiwa katika eneo husika. Kuna siri za kufaulu mitihani shuleni, kuna siri za kuwa na familia bora na kadhalika. Naita siri lakini kiukweli sio siri kwani ni vitu ambavyo tunavijua ama tunaona kwamba havina maana katika maisha yetu na hivyo kutotilia maanani.

Labda nianze kwa kukuuliza swali hili; Ikiwa una ndoo ya maji iliyojaa maji tayari, ukitaka kuweka kitu kingine katika ile ndoo au maji mengine utafanyaje? Majibu yanaweza kuwa mengi lakini jibu la muhimu ni kuyatoa yale maji kwa kumwaga ama kumpa anaehitaji ili upate nafasi ya kuweka kitu kingine. Lakini litakuwa sio jambo jema kumwaga maji wakati kuna anaehitaji. Kwa hiyo basi siri ya kupokea kitu chochote ni kutoa, ndio kutoa kwa anaehitaji ili nawe upate nafasi ya kupokea kitu kipya. Kama hutatoa na wewe umeshajaza vitu katika sehemu yako ni dhahiri kwamba hakutakuwa na nafasi ya kupokea kitu kipya. Ndio maana tunashauriwa kutoa ili nasi tupokee, huwezi kuwa mtu wa kupokea pekee.


Tunapozungumza suala la utoaji tunamaanisha kitu chochote ambacho kinaweza kuwa msaada kwa mtu mwingine. Suala la kutoa sio lazima uombwe, ni muhimu zaidi kama ukitoa bila msukumo kutoka nje. Kitabu cha biblia kinawaasa watu kuwa kutoa ni bora kuliko kupokea na pia utapokea kadiri nawe unavyotoa, tena maradufu. Unapozungumzia suala la kutoa watu wengi hupeleka akili zao katika pesa. Kutoa pesa ni muhimu pia, lakini je kama huna pesa huna sifa ya kutoa? Unaweza kutoa kitu chochote kwa mtu yeyote ilimradi kina msaada kwake. Unaweza kutoa msaada, kutoa elimu, kusaidia wasiojiweza, kufundisha wenzako, kutoa muda wako kwa kusaidia wengine ama kuwatembelea wagonjwa, yatima na wale wanaohitaji faraja na hata kutoa sehemu ya mali zako kwa wengine. Kuna siri kubwa katika utoaji, ni siri ambayo haiwezi kuelezeka kirahisi ni siri kubwa sana ya kupokea chochote. Ila muhimu sana ni kwamba unapotoa kitu usitoe ukingoja shukrani au ukitegemea malipo kwani malipo yake utapata katika muda usioutegemea tena kwa mtu usiyemtegemea. Kuna msemo wa Kiswahili usemao ‘’Tenda wema nenda zako, usingoje shukurani’’.
Soma: Je umepanda nini shambani kwako?

Ndugu yangu unaesoma hapa nawe una kitu cha kutoa kwa watu wengine, usiwe mtu wa kupokea pekee bila kutoa. Kutoa hakukufanyi kufilisika bali kuendelea kuneemeka. Kama kutoa kungekuwa kunafilisi basi bilionea tajiri namba moja duniani Bill Gates angeshafilisika kitambo kwa misaada  anayotoa duniani kupitia mfuko wake wa Bill and Melinda Gates unaohusika kutoa misaada kwa watu masikini kote duniani. Kwa hapa nyumbani Tanzania basi mzee Reginald Mengi angekuwa ameshafilisika kitambo pia maana toka nilivyoanza kumsikia anatoa misaada kwa kweli angekuwa ameshaishiwa. Bilionea namba tatu kwa sasa ambae pia alishakuwa namba moja na mbili katika kipindi cha nyuma Warren Buffet nae ni mtoaji mzuri na amedhamiria kutoa 99%  ya utajiri wake kama misaada katika maisha yake yote. Hii ni tofauti kabisa na dhana hasi iliyojengekwa kwamba watu matajiri ni wabinafsi na wachoyo, jambo ambalo si kweli. Matajiri hupenda kusaidia hasa wale wanaonyesha nia ya kufanya jambo fulani zuri.

Kama wewe ni mwanafunzi na unalijua vizuri somo fulani kuliko mtu mwingine yeyote darasani kwako ukiamua kulifundisha hilo somo kwa wengine, si tu kwamba utakuwa umewasaidia wengine kufaulu somo linalowapa shida bali pia nawe utaimarika katika hilo somo kwa kupokea changamoto na kupokea elimu mpya kutoka kwa wengine.Pia itakusaidia kukumbuka kirahisi na kuonekana bingwa wa somo husika. Utafungua mlango wa wenzako kukusaidia katika masomo mengine ambayo wanayaweza vizuri kuliko wewe. Kinyume chake ni kwamba hutaona mafanikio mazuri katika masomo yako kama utakuwa mbinafsi. Kila mtu anaweza kutoa kitu, hata kama ni kidogo kiasi gani. Ndio maana hata katika dini zetu tunasisitiziwa kutoa zaka katika nyumba za ibada kama shukurani kwa Mungu wetu kwa aliyotujalia kupata.

Inaweza kukuwia vigumu pale unapoanza lakin utaweza kuzoea tabia hiyo ya utoaji kadiri unavyotoa kila mara. Unaweza kuanza kidogo kidogo mpaka pale utakapoona kwamba sasa huoni ugumu katika kutoa. Labda nikupe hadithi ya kweli; Mwaka fulani nikiwa sekondari, tulitoka shule mchana kama ilivyo ada. Tukitembea watatu njiani kuelekea nyumbani mmoja wetu (si mimi) alitoa kiasi fulani cha pesa kwa mlemavu aliekuwa anaomba barabarani, hatua kama tano mbele aliokota mara tano ya pesa aliyotoa kwa yule mlemavu. Unaona katika mfano huu jinsi kutoa kunavyofungua milango mingine, milango ya kupokea. Sikuambii kwamba ukitoa nawe utaokota hela kama rafiki yagu,hapana. Toa kwa kuwa umeguswa na ukiamini kwamba unawasaidia wengine kwa kile ambacho umejaaliwa kuwa nacho. Tahadhari tu kwa upande wa fedha uweze kutofautisha kati ya kutoa kusaidia na kutapanya pesa zako ovyo. Unaweza kuanza kwa kutenga asilimia ya mapato yako kwa kusaidia wengine. Muda wako nao ni wa thamani sana hivyo ni muhimu kuulinda na kutoutoa kwa wale wasiostahili.

Usisahau kupenda ukurasa wetu wa facebook kwa kubonyeza Pambazuka Daima Blog na pia kujiunga na orodha yetu ya barua pepe kupata makala kila mara zitokapo.

Nickson Yohanes
nmyohanes@gmail.com
Acha kulalamika kuhusu kazi yako na fanya mambo haya mawili.

Acha kulalamika kuhusu kazi yako na fanya mambo haya mawili.

Ndugu msomaj habari za siku ya leo. Nakukaribisha katika makala ya leo.
Ajira kwa sasa ni changamoto kubwa sana hasa hasa kwa vijana na pia katika nchi zinazoendelea hasa dunia ya tatu. Si tu katika kuipata bali pia katika kuifanya.
Labda nianze kwa kukueleza kuwa tangu nikiwa mwanafunzi mpaka sasa nimebahatika kukutana na wafanyakazi wengi ambao wamekuwa wakilalamika kuhusu kazi zao, nazungumzia katika kada nyingi nilizobahatika kukutana nazo hasa wafanyakazi wa ngazi ya chini na kati. Kila mtu analalamika kuhusu kitu ambacho yeye anakikosa anatendewa. Lakini wengi wamekuwa wakilalamika kuhusu maslahi duni (mishahara na marupurupu), mazingira magumu ya kazi, manyanyaso kutoka kwa wakubwa wao wa kazi, kudharaulika, kupuuzwa na hata kutokusikilizwa na mengine yanayofanana na haya.

Mbali na kwamba tatizo linaweza kuwa kwa wanaolalamikiwa kwa kutotekeleza majukumu yao pia kuna wafanyakazi wasiotekeleza majukumu yao. Hilo tatizo pia tatizo kubwa ni kwamba wafanyakazi wengi wamekuwa watu wa kulalamika bila kuchukua hatua. Unakuta mtu kaajiriwa mwanzoni mwa miaka ya tisini bado analalamika kuhusu hali aliyoikuta bila yeye kashindwa kuibadili au yeye mwenyewe kubadillika. Kulalamika na kulaumu kamwe hakuwezi kutatua tatizo lako kazini bali kuchukua hatua pekee ndio njia ambayo inaweza kusaidia. Kuna hatua kadhaa ambazo utatahitaji kuchukua kama mfanyakazi ambaye unaona hautendewi inavyopasa.

Hatua ya kwanza ni kubadili mtazamo kuhusu kazi unayoifanya. Jitathmini na kuweza kugundua wapi kuna tatizo kati yako na mwajiri wako. Yawezekana kuna matatizo kidogi kwenye ajira yako kulinganisha na wewe unavyochukulia. Mapungufu hayawezi kukosekana popote hivyo mengine yapasa uyazoee na kuchukulia kama sehemu ya changamoto za kazi. Matatizo mengi yanaanza kwenye mtazamo wako (attitude) kuhusu jambo fulani. Kama ukijenga mtazamo hasi basi utaona kila kitu ni kibaya lakini ukiojenga mtazamo chanya utaona mazuri kuliko mabaya. Kama pia wewe ni muoga kuchukua hatua ambayo nitaitaja hapa chini basi bora ukubaliane na kazi yako na kuamua kuifanya kwa moyo wako. Wengine ni waoga sana kuchukua hatua hiyo, huwaza wataishije. Jipime na uangalie kama unaweza kubadili kitu kibadili na kama huwezi kubadili kubaliana na hali halisi iliyopo.

 Kubadili kazi yako kwa kufanya kazi nyingine. Ndugu yangu hii ni hatua ngumu sana kwa watu walio wengi hasa ambao wamekaa kwenye ajira kwa muda mrefu na pia wana majukumu mengi. Najua ilivyo ngumu sana kuacha kazi ambayo ndiyo ilikuwa kila kitu kwako lakini kama haikupi yale ambayo ulikuwa ukiyapata kabla huna budi kujikaza na kuchukua hatua hii. Mwanafizikia maarufu zaidi wa karne ya 20 aliwahi kusema kwama kuendelea kufanya kitu kile kile kwa namna ile na kutegemea matokeo tofauti ni ujinga. Kwa mfano umekuwa ukilipwa hela ndogo sana kiasi kwamba huwezi hata kujiwekea akiba ama hautoshelezi kiasi kwamba unaweza kuwa unaishi kwa madeni tu na wakati huo ukitegemea kufanikiwa katika kujiletea maendeleo utakuwa ni zaidi ya muujiza. Sisemi kwamba wote wanaoshindwa kujiwekea akiba kunatokana na kulipwa hela ndogo, la hasha kuna wengine wanshindwa kujiwekea akiba kutokana na matumizi yao mabovu ya hela. Ila kuna wengine kweli ni ngumu kujiwekea akiba kwa vipato vyao vidogo na majukumu mengi. Suluhisho hapo ni kutafuta kazi nyingine unayoipenda kabla hujaacha uliyonayo ama kuanza kufanya shughuli nyingine tofauti na ajira yako yaani kujiajiri au ujasiriamali. Pia kuna mtu aliwahi kusema Kama kile unachofanya hakikupi tena faida ni bora kukiacha. Kunahitaji ujasiri mkubwa sana kwa baadhi ya watu kuacha kazi. lakini kabla hujaogopa kuacha kazi, jaribu kujiuliza itakuwaje siku ukifukuzwa kazi? Je utaishije, je utakufa? naomba ujijibu mwenyewe. Tatizo la wafanyakazi wengi ninkwamba hawajiandai kustaafu tokea siku ya kwanza ya ajira. Kumbuka huna uhakika na ajira yako maana huhusiani moja kwa moja na mwajiri wako kiasi kwamba utafanya kazi hiyo mpaka ufikie umri wa kustaafu kwa lazima. Hivyo basi ni muhimu kujipanga kabla hujapangwa. Ni bora kabisa uanze kutafuta vyanzo vingine vya mapato kwa kujiajiri, kufanya biashara au ujasiriamali wakati ukiendelea na kazi unayoifanya ili ikitokea umeacha basi uwe na pa kuanzia.
Soma: Je umepanda nini shambani kwako?

Wengine huogopa kuacha kazi kwa sababu hawana akiba yoyote waliyojiwekea. Yaani maisha yake ni kula tu yaani anafanya kazi aishi, waingereza husema Living hand to mouth. Ndugu yangu ukiishi hivyo ujue kwamba hakika utakufa masikini. Sikutabirii ila ndio ukweli wenyewe huo. Mtu mmoja aliwahi kuniambia usiishi kama mvuvi (samahani wavuvi), kwani wavuvi walio wengi hawaamini katika kujiwekea akiba maana anajua ziwa, mto ama bahari wanakovua zipo milele na atavua tu. Tabia hii huwafanya watumie mapato yao vibaya na kushindwa kujisaidia wakati ambapo hawana nguvu, wagonjwa, wamezeeka ama hakuna tena samaki kwa kipindi fulani au serikali kusitisha uvuvi ili kuruhusu samaki kuzaliana.

Nipende kuhitimisha tu kwa kukuambia kuwa kuendelea kulaumu, kunung´unika ama kulalamika hakutasaidia kama wewe hujaamua kutafuta suluhisho. Kumbuka kwamba maisha ni yako na mfanya maamuzi ni wewe. Ukiamua kuendelea kulia ni sawa pia na ukiamua kuchukua hatua ni bora zaidi. Changamoto ni sehemu ya maisha na uchaguzi ni wako uishije, mfano unaweza kuhainga sasa hivi ukaishi vizuri kesho ama uishi kwa starehe leo ukahangaike kesho.
Nyakati ngumu hazidumu lakini watu wagumu hudumu (Tough times never last but tough people do),nimenukuu kutoka kwa mwandishi Robert H.Schuller.
Nakutakia siku njema, kwaheri.

Nickson Yohanes
Email: nmyohanes@gmail.com

Ili uweze kupata mafanikio ni lazima ulipe gharama hizi

Habari za muda huu ndugu msomaji wa mtandao huu wa PAMBAZUKA DAIMA, natumaini kuwa hujambo na unaendelea vyema na harakati za kujiletea maendeleo , kama hauko vyema basi pole na kumbuka kuwa hizo ni changamoto za maisha ambazo tunazipitia.

Je unalipa gharama za mafanikio?
Hili ndilo swali ambalo unatakiwa kujiuliza kabla hujaendelea mbele, kisha fuatana nami hapa chini ili tusome kwa pamoja.
Neno mafanikio ni neno linalovutia sana kulisikia masikioni, najua kwanini ni kwa sababu kila mtu ananyatamani na kuwaza kuyafikia mafanikio. Kuna mafanikio yapo katika nyanja zote kama afya, elimu, fedha na hata kiroho. Mafanikio huja kwa njia nyingi na namna mbali mbali lakini kuna kanuni kubwa ya kuweza kufanikiwa. Kanuni hiyo ni kulipa ghara za kufanikiwa. Hakuna yeyote alieyewahi kufanikiwa bila kulipa gharama zinazotakiwa kuweza kufanikiwa. Kama unataka kufanikiwa basi kuwa tayari kulipa gharama hizo. Wengi hujaribu kukwepa kulipa gharama na kuamua kutumia njia ya mkatio ya kutafuta mafanikio. Ukweli ni kwamba hakuna njia ya mkato bila kulipa gharama, na mara nyingi ukijaribu kukwepa gharama utajikuta unalipa gharama kubwa sana baadae.


Miongoni mwa gharama za kulipa ni muda wako. Ni lazima uwekeze muda wako katika kile ambacho unakifanya. Kwa mfano kwa mwanafunzi itamlazimu yeye kuutumia muda wake mwiingi kwa kusoma na kujiandaa na mitihani na kwa upande wa mkulima atautumia muda wake mwingi kuhudumia shamba lake. Lazima uutenge muda wa kutosha kwa shughuli ama jambo lile ambalo umepanga kulifanikisha. Tumia muda wako vizuri maana huwezi kuulinda muda bali unaweza kuutumia vyema, kumbuka tu kwamba kila mtu ana saa 24 tu na hakuna mwenye zaidi ya hapo. Matumizi mazuri ya muda wako kwa kuwekeza katika kile cha kuweza kukuletea mafanikio ndiyo yatayokutofautisha wewe na wale ambao hawajafanikiwa. Usiutumie muda wako katika vile vitu ambavyo si muhimu na havikusaidii kusonga mbele kuelekea kwenye mafanikio kama muda mwingi wa kupiga soga, kutumia muda mwingi katika mitandao ya kijamii na kuzurura.

Gharama ya kufanya kazi kwa juhudi na maarifa, huu ni ukweli ambao lazima sote tuujue. Huwezi kufanikiwa kama hufanyi kazi, tena ufanye kazi kwa juhudi na maarifa. Sio nguvu peke yake bali maarifa pia lazima yawepo maana kuna watu wengi sana ambai ni hodari wa kufanya kazi lakini ni masikini wa kutupwa. Lazima ujue ni wapi hasa pa kuwekeza juhudi zako. Mbali na hilo ni lazima pia ujiongezee maarifa kupitia njia mbalimbali mfano kusoma sana vitabu. Maarifa mengi tuyatakayo yapo kwenye vitabu, yameshaandikwa tayari. Pia kuhudhuria semina na matamasha yanayokuongezea maarifa katika kile unachofanya. Kwa mfano wewe ni mfanyabiashara unaweza kuhudhuria semina za kukuza mitaji, uwekezaji na hata mauzo.

Uvumilivu ni gharama nyingine ambayo unatakiwa kuilipa. Kama ukitaka kufanikiwa kweli ni lazima uweze kulipa gharama hii. Uwezo wa kuweza kuvumilia ndio utofauti wa kipekee uliopo miongoni mwa waliofanikiwa na wasiofanikiwa. Watu wengi wenye kuvumilia kuyasubiri mafanikio huku wakiendelea kujituma ni dhahari kuwa watafanikiwa. Usiwe na tamaa ya kupanda na kuvuna kesho, Mfikirie mkulima wa miti ambae hupanda miti na kusubiri zaidi ya miaka minane, kama sio mvumilivu asingeweza kuipanda miti hiyo. Kuna dhoruba nyingi kufika huko lakini huna budi kuvumilia kama kukatishwa tamaa, kuanguka na kadhalika lakini huna budi kufika kileleni. Kumbuka tena hakuna njia rahisi wala ya mkato ya kuyafikia mafanikio isipokuwa kwa kuilipa gharama. Jiwekee lengo kwamba utafanikiwa na lazima utafanikiwa tu.

Gharama za fedha, fedha ni muhimu sana tena sana. Pesa ni mtumishi mwema sana ambaye anaweza kukufanyia kazi zako na kukuletea faida. Hakuna mtu hata mmoja ambaye anasema pesa sio muhimu. Utahitaji fedha ili uweze kuwekeza, kufanyia biashara, kuisha na mengine mengi ambayo unayajua kuhusu fedha. Kuwa tayari kulipa gharama za kifedha kuweza kufanikiwa. Wekeza pesa ili uweze kufanikiwa ili uweze kupata faida pia.

Kujitoa sadaka (self-sacrifice), Hili ni la lazima sana kuweza kufanikiwa. Hakuna njia nyingine ndugu lazima ujiotoe sadaka, lazima ukubali kuyasotea mafanikio yako. Mwanzoni mambo huwa magumu sana hata kukufanya ukate tamaa. Uvumilivu na imani kubwa ni muhimu sana kwa kipindi hiki. Bondia maarufu sana dunia marehemu Muhammad Ali aliwahi kusema ``Niliichukia kila dakika ya mafunzo lakini nikasema ´Usiondoke´Teseka sasa ili uishi maisha yako yote kama mshindi´´. Ni lazima ujitoe kweli kweli, ni lazima uamue kutafuta kile unachokitaka. Mafanikio sio rahisi ndio maana sio watu wengi wamefanikwa. Ni lazima uamke mapema, ni lazima ufanye kazi hata kama hupendi, lazima kujifunza, lazima uchelewe kulala wakati mwingine, kujinyima baadhi ya vitu, kutokubali kukatishwa tamaa na vingi vingine.

Upendo nao ni gharama nyingine ya kulipa, unaweza kuiona ndogo lakini si kweli. Utahitajika kuwapenda maadui zako, wabaya wako, washindani wako na hata washindani wako. Utahitaji kuwapenda watu ili ujifunze kutoka kwao, sio upendo wa usoni tu bali ni upendo kutoka moyoni. Yakupasa pia upende unachokifanya, ukipenda unachokifanya utakifanya kwa moyo wako. Kama bado hujapata unachokipenda jaribu kukitafuta. Hata kama mtu anakuchukia sio lazima na wewe umchukie.

Kufanya vihatarishi (Take risks), watu wengi wanaogopa kuthubutu. Wanaogopa kujaribu kufanya kitu kipya kwa kuhofu kuhusu hatari zilizopo katika kitu hicho. Wako tayari kuendelea kuwa katika hali waliyonayo badala ya kujaribu kuchukua hatua. Ni bora zaidi kufanya kitu cha kuhatarisha kuliko kukaa bila kufanya chochote.Ni hatari zaidi kukaa bila kufanya vihatarishi kuliko kufanya. Watu wengi hawajutii vile vitu ambavyo wamevifanya hata kama walishindwa bali vile ambavyo hawakufanya. Utafiti uliofanyika unaonesha kwamba wale watu wanaothubutu kufanya vitu vya hatari hushindwa mara chache zaidi kuliko kufanikiwa.

Katika vita vya pili vya dunia marubani wa ndege za kivita waliokuwa tayari kukabili hatari waliweza kuokoa maisha yao kuliko wale ambao walikuwa wakijihami zaidi na kuogopa kukabili hatari. Utafiti mwingine unaonyesha kwamba wale watu ambao huishi kwa tahadhari sana huishi muda mfupi kuliko wale wanaojiingiza katika hatari. Kufanya vitu hatarishi haimaanishi kufanya vitu vya hatari ovyo, siku zote fanya hatari ambazo umeshazipigia mahesabu, Waingereza wanasema take calculated risks.
Nakuatakia utekelezaji mwema.

Nickson Yohanes
Email: nmyohanes@gmail.com

Choma meli yako sasa

Ndugu msomaji napenda kutumia wasaa huu kuweza kukusalimia kabla sijaanza kukushirikisha niliyonayo leo. Nianze kwa kukusimulia hadithi moja:

Hapo zamani kuna kiongozi wa nchi fulani alienda vitani na jeshi lake katika nchi ya kigeni kwa kutumia usafiri wa meli. Alipofika pwani ya nchi ya adui aliamuru jeshi lake kuchoma meli waliyokwenda nayo. Aliwaambia wapiganaji wake kwamba kwa sasa wana machaguo mawili tu ambayo ni kushinda ile vita na ni lazima washinde ama kufa wote kwani hawawezi kutoka salama huko kwa kutoroka kwani wameshachoma moto meli yao. Wasiposhinda maana yake watauawa ama watakuwa mateka ama washinde vita na warudi nchini kwao salama. Hapo sasa kukawa hakuna jinsi zaidi ya jeshi lake kuwa na dhamira moja tu ya kushinda kwani kwani kwa namna yoyote hawako salama maana wakipigana wanaweza kushinda lakini pia wanaweza kufa na wasipopigana pia wanaweza kufa kwa hiyo walijitoa kwa

Hizi ndizo kanuni za kuwa na afya bora

Ili uweze kufanya shughuli zako za kila siku ikiwa ni pamoja na shughuli za uzalishaji mali ni lazima uwe na afya njema. Afya ni hali ya kuwa vizuri kimwili, kiakili, kisaikolojia na kiroho pia. Watu wengi huchukulia kuwa watu wanene ndio wenye afya njema na wakati mwingine hudhani kuwa watu wembamba ndio wenye afya. Lakini kiukweli hilo si kweli.  Mtu mwenye afya ni yule mwenye sifa nilizotaja hapo juu.

Kama huna mojawapo kati ya hivi basi hatuwezi kusema kuwa una afya njema. Ukiwa na afya njema utaweza kuishi maisha yenye furaha na amani na pia utaweza kujizalishia kipato chako kwa kila siku iendayo kwa Mungu. Ili uwe na afya njema inakupasa

Faida za kiafya zitokanazo na ulaji wa ndizi mbivu

Ndizi mbivu ni tunda lilotokanalo na mmea wa mgomba. Katika nchi yetu ya Tanzania kuna mikoa ambayo imebarikiwa kuzalisha ndizi kwa wingi. Mikoa hiyo ni Arusha, Kagera, Kilimanjaro, Mbeya na Morogoro. Ndizi zina rangi ya kijani zinapokuwa mbichi na njano zinapoiva na hivyo kuwa na rangi ya kuvutia. Ndizi pia zina ukubwa na maumbo tofauti tofauti. Ndizi mbichi hutumika kwa chakula kwa kupikwa na kuchanganywa na vyakula vingine kama nyama, maharage na samaki ila zikivumbikwa na kuiva hutumika kama tunda. Baadhi ya makabila hutumia ndizi mbivu kutengeneza pombe za asili kama lubisi na mbege. Pia kuna viwanda vya kisasa vinavyotumia ndizi kutengeneza mvinyo (wine). Kuna aina nyingi za ndizi lakini faida zake mwilini zinafanana.

Zipo faida kadhaa zinazotokana na ulaji wa ndizi mbivu. Faida hizo ni kama kudhibiti kiasi cha sukari mwili na pia kufanya mwili kutengeneza kemikali maalum za kufanya mwili kupumzika/kupunguza msongo. Faida nyingine ya ndizi mbivu ni uwezo wake wa kuweza kupunguza uvimbe katika sehemu ya mwili, kuzuia aina ya pili ya kisukari (type II diabetes), kupunguza uzito hasa kwa kuwa ndizi zina kiwango kikubwa cha nyuzi nyuzi (fibres), kuimarisha mfumo wa fahamu na kusaidia katika utengenezajiwa chembe nyeupe za damu (white blood cells) ambazo hupambana na magonjwa mwilini hasa kutokana na kuwa na kiwango kikubwa cha vitamini B-6.
SOMA: Namna bora ya kupungiuza uzito
Pia ndizi mbivu husaidia kupunguza sononeko (depression) kutokana na kuwa na kiwango kikubwa cha tryptophan ambayo hubadilishwa kuwa serotinin ambayo ni kihamasishi cha kutoa furaha katika ubongo. Mbali na faida hizo ndizi huoingeza nishati mwili kwa kuwa na wanga na sukari, huongeza damu kwa kuwa na madini ya chuma na hivyo kukuepusha na ugonjwa wa upungufu wa damu maarufu kama anaemia. Ndizi pia husaidia pia katika umeng`enyaji wa chakula (digestion) na kusaidia kupambana na sumu ziingiazo mwili kupitia vyakula mbalimbali.
Faida zingine zinazotokana na tunda hili maarufu ni husaidia kuupa utumbo afya kwa kuruhusu kuzaliana kwa bakteria wazuri ambao hufanya kazi mbalimbali mwili maarufu kama prebiotiki na husaidia pia katika utengenezaji wa vimeng`enyo kwaajili ya umeng`enyaji wa chakula mwilini. Kama vile haitoshi ndizi pia husaidia pia kupunguza maumivu ya vidonda vya tumbo kwa kufunika utumbo dhidi ya tindikali zichubuazo utumbo kama Haidrokloriki. Ndizi hutumika kupambana na kemikali zisizotakiwa mwilini au sumu (antiodixants) na pia kupambana na baadhi ya magonjwa sugu. Ndizi zina kiwango kikubwa cha madini ya magneziam na vitamini B ambayo husaidia kuacha uvutaji wa sigara.

Faida zingine ambazo hutokana na ndizi ni kusaidia afya ya akili hasa kumbukumbu na kujifunza, kusaidia tumbo kufanya kazi vizuri kutokana na kuwa na kiwango kikubwa cha cha nyuzi nyuzi (fibres), kupunguza kichefuchefu na kusaidia afya ya macho kwa kuzuia uharibifu wa misuli ya macho .Pia ndizi huzuia saratani ya figo na kuimarisha mifupa hasa kutokana na kuongeza uwezo wa mwili kuchukua madini ya kalsham kutoka kwenye vyakula vingine. Mwisho ndizi husaidia kurudisha chumvichumvi na sukari ipoteayo mwilini kutokana na ugonjwa wa kuendesha (diarrhea).
Naamini kuanzia sasa utaongeza ulaji wako wa ndizi mbivu ili kupata faida hizo zaidi ya kumi nilizoziainisha hapo juu. Kumbuka nyumba hujengwa kwa tofali, miti na zege lakini mwili wenye afya njema hujengwa kula vyakula bora.
Usisahau kumshirikisha mwenzako.
Makala hii imeandaliwa na kuandikwa na:
Nickson Yohanes
nmyohanes@gmail.com

Madhara ya kutumia mifuko ya plastiki (rambo) kubebea vyakula vya moto

Habari za wakati huu ndugu msomaji wa makala zangu katika mtandano huu wa PAMBAZUKA DAIMA ni matumaini yangu kwamba uko bukheri wa afya, na kama kwa vyovyote vile hali yako ya kiafya siyo ya kuridhisha basi nakupa pole na kukuombea upate nafuu na upone haraka.

Ndugu msomaji kumekuwepo na tabia ya watu wengi kupuuzia vitu ambavyo vina madhara kidogo ama ambavyo huchukua muda mrefu kuliko vile ambavyo vinaonyesha madhara katika muda mfupi. Vitu ambavyo vinasababisha ugonjwa papo hapo ama baada ya muda mfupi huchukuliwa kwa umakini mkubwa kulinganisha ni vile ambavyo vinachukua muda mrefu kusababisha ugonjwa.


Leo ningependa kidogo kuzungumzia vifungashio (packages) vya vya chakula ambavyo vimekuwa vikitumiwa na wetu wengi hasa kubebea vyakula vya moto kama chipsi. Vifungashio hivyo si vingine bali ni mifuko ya plastiki maarufu kama mifuko ya rambo. Ukiangalia kwa jicho la kawaida hutaweza kuona madhara yake moja kwa moja hasa kutokana na kwamba huchukua muda mrefu kuja kuona madhara yake ni hivyo watu wengi kutokutilia maanani na mazoea pia ya matumizi ya mifuko hiyo kwenye jamii zetu.

Mitaani na maeneo hasa ya vyuo vikuu kumekuwa na mazoea ya kubeba vyakula vya moto hasa chipsi wakiwa na lengo la kwenda kulia sehemu nyingine mbali na sehemu vinapouzwa.
Mifuko ya plastiki inapopigwa na joto mkali au mdogo kwa muda mrefu hutoa kemikali ambazo huingia kwenye chakula na hivyo kuingizwa mwilini kwa njia ya kula. Kama kemikali hizo zitaendelea kuingizwa kwenye mwili zitaendelea kujijenga mwilini na hivyo kumuweka mlaji katika hatari ya kuugua ugonjwa wa saratani (kansa). Ugonjwa wa kansa kama mjuavyo hauwezi kuanza kama malaria bali huanza kidogo kidogo na mpaka uje kuonekana basi utakuwa umeshambaa sana mwilini. Hatari iliyopo katika mifuko hii si kwa vyakula vya baridi bali vyakula vya moto ambavyo hufanya kemikali hizo kuyeyuka na kuingia kwenye chakula. Kemikali hizo zinajulikana kama Polyvinyl Chloride, polyethylene, polystyrene, styrene na bisphenol.

Mbali na kuongeza uwezekano wa kuugua saratani pia madhara mengine yanayohusishwa na matumizi ya mifuko ya plastiki kubebea vyakula vya moto ni kubadilika kwa jeni za mwili, kuharibika kwa jeni za mwili, matatizo ya uzazi, matatizo ya moyo na matatizo ya kushindwa kuweka katika msawazo (urari) vichocheo mbalimbali vya mwili (homoni) ambavyo husaidia ufanyaji bora kazi wa mwili na hivyo kuathiri baadhi ya tabia hasa kwa watoto.

Kama hakuna ulazima wa wewe kutumia mifuko ya plastiki kubebea vyakula vya moto basi acha kabisa maana matumizi yake. Wahenga walisema ´bora kinga kuliko tiba´, hivyo basi ni bora kuzuia tatizo linalozuilika sasa ili kuepuka madhara ya kesho. Ni imani yangu kwamba utaweza kupunguza matumizi ya mifuko ya rambo katika kubebea vyakula vya moto na hatimae kuacha kabisa. Najua sio jambo rahisi hasa kama umeshazoea lakini ukiamua utaweza kabisa kuacha matumizi hayo.
Nikutakie utekelezaji mwema.

Nickson Yohanes
Email: nmyohanes@gmail.com

Wanaobebeshwa lawama hizi, hawastahili kuzibeba

Malezi kwa watoto yamekuwa changamoto kubwa sana katika dunia hii ya sayansi na teknolojia tena dunia inayokwenda kwa kasi sana mithili ya roketi, dunia iliyojaa kila aina ya changamoto. Imekuwa ni kawaida sasa kusikia watu wazima wakiwalalamikia vijana ama watoto kuwa wamekuwa na tabia ambazo si nzuri hasa kulinganisha na wakati wao. Siwapingi lakini nani wa kulaumiwa, je mtoto, mzazi au jamii?.


Kabla sijamtaja mtu wa kulaumiwa (japo sishauri hivyo) nikumbushe kuwa mtoto huzaliwa akijua vitu viwili tu kulia na kunyonya na kuanzia hapo huanza kujifunza kidogo kidogo hasa kwa picha ama matendo. Baadae ataanza kujifunza maneno afikapo umri wa kuongea na hata kusoma na kuandika akibahatika kuhudhuria shule. Sasa swali la kujiuliza ni kwamba mtoto anajifunza haya kutoka kwa nani?. Bila shaka ni kutoka kwa watu waliomzunguka, baba, mama, wakubwa zake ,majirani,ndugu, jamaa na marafiki ambayo hiyo tunaita jamii yake. Katika jamii hii atajifunza mazuri na hata mabaya yaliyopo ndani ya jamii yake. Bahati mbaya au nzuri ni kwamba katika kipindi cha kujifunza mtoto hawezi kuchagua cha kujifunza na cha kuacha kwani hana uwezo huo. Pia ni kipindi ambacho yeye huwa na uwezo mkubwa wa kuhifadhi vitu vingi na pia kuwa uwezekano mdogo wa kuyasahau. Hivyo basi chochote ambacho mto huyu atajifunza basi kitanasa kichwani kwa muda mrefu na kiasi kwamba anaweza kufikia umri wa utu uzima na bado akaendelea kukumbuka yaliyotokea utotoni. Hivyo basi malezi ya mtoto hasa katika kipindi chake cha udadisi ni cha muhimu na inabidi jamii yake iwe makini kwani ndicho kipindi ambacho wanaweza kumtengeneza raia mwema ama raia mbaya wa Taifa husika, kipindi ambacho chaweza kumjeruhi mtoto husika.

Kama nilivyotangulia kusema katika aya iliyotangulia ni kwamba mtoto hujifunza kila kitu kutoka kwa watu waliomzunguka (jamii na wazazi) hivyo basi mtoto hapaswi kulaumiwa kwa tabia aliyo nayo bali kufundishwa na kuonywa ama kuadhibiwa inapobidi. Ni rahisi zaidi mtoto kujifunza kwa kuona kuliko kuambiwa. Mathalani mtoto amelelewa katika mazingira ya ubabe halafu wazazi au walezi wake wanamwambia kwamba awe mpole, haiwezekani!. Hawezi kujifunza asichokiona, hajui upole unafananaje na una faida gani. Mzazi kutwa unashinda kutakana watoto wako wanapokosea halafu utegemee watoto wako wasitukane watakapokosewa, itakuwa ni jambo gumu sana kwake maana ndivyo alivyofunzwa kuishi.

Mzazi jitahidi kuishi yale maisha ambayo utataka mwanao aje kuyaishi. Kama unapenda wanao wapende kusoma, basi kuwa mfano bora katika kusoma na sio kuishia tu kuwaamrisha kusoma. Mtoto hajawahi kukuona unashika kitabu hata cha dini yako halafu yeye kutwa unamhubiria kufanya hivyo. Nakuhakikishia atachukua kitabu na kukikodolea macho, kuhesabu kurasa lakini kamwe hatasoma na ukitoka tu na yeye ataweka kitabu chini. Tusiigize maisha, kama unapenda kuangalia TV tegemea hilo kutoka kwa mwanao pia. Kwani hujawahi kusikia watu wakisema `mtoto wa fulani yuko kama baba ama mama yake?´ Ni kwamba tabia za watoto ni picha ya familia wanazotoka, ni mabalozi wa familia zao popote watakapokwenda. Usiwe tabia zile ambazo hupendi mwanao awe nazo na hazikuwakilishi vyema katika jamii.

Changamoto kubwa iliyopo pia ni wazazi kutingwa na kazi (busy) kiasi kwamba jukumu la malezi limeachwa kwa msaidizi wa ndani maarufu kama yaya ama Housegirl kwa kiingereza. Kama msaidizi huyo akiwa na tabia njema anaweza kulea vizuri lakini japo sio jukumu lake kulea muda wote. Yeye anapaswa kukusaidia tu katika kipindi ambacho haupo nyumbani. Ukirudi kutoka kazini mlee mwanao walau ajue kwamba wewe ni baba au mama, watoto wengine wamelelewa na wasaidizi kiasi kwamba humsahau mama na kudhani wale wasaidizi ndio mama zao na mama zao huwaita dada, msifike huko. Tekeleza jukumu lako kama mzazi na kama ukiona haupo tayari kulea basi usiwe na mtoto mpaka utakapokuwa tayari kulea. Kama msaidizi akiwa na tabia mbaya (wakati mwingine kutokana na anavyoftendewa na bosi wake) basi mtoto huuvuna huo ubaya maradufu na hata wakati mwingine kudhuriwa. Kwani kesi kama hizo hujasikia? Zipo nyingi tu siku hizi. Sisemi usiwe na msaidizi wa kazi, bali usimwachie yeye jukumu la kulea peke yake, hilo ni jukumu lako wewe mzazi (baba na mama).

Pia nitumie fursa hii kukukumbusha tena kwamba ufanye yale ambayo unaona yanafaa kwa mwanao na atajifunza kutoka kwako na atakuwa mtu bora na raia mwema. Tabia nyingi alizonazo mtoto amezipata kwenye jamii yake. Na kama mtoto wako ataanza kuwa na tabia ambazo huzipendi na wewe huzifanyi, tafuta chanzo cha tabia hizo mfano udokozi, matusi na tabia zinazofana na hizo na kumtenga na chanzo hicho kama hatua ya kwanza na pia kumkanya hata kumuadhibu pale inapobidi ili ajue kuwa kafanya kosa alijutie kosa hilo. Kwa wasomaji wa Biblia watakubaliana na mimi kuwa kuna mstari unaosema mlee mtoto katika njia impasayo naye hataiacha hata atakapokuwa mzee. Pia kuna msemo wa Kiswahili usemao mtoto umleavyo ndivyo akuavyo. Ukimlea vyema atakua vyema na ukimlea vibaya atakua vibaya. Usikubali mwanao awe balozi mbaya kwako na usiubali apatikane raia mbaya wa nchi yako. Jamii yetu isikae kimya na kushindwa kukemea mabaya ambayo wanayaona kwenye malezi ya watoto wa jamii zetu. Mke wa rais mstaafu wa awamu ya nne aliwahi kusema Mtoto mwenzako ni wako, na wa kwao pia ni wako. Kwa pamoja tuwalee ili tujenge taifa bora la sasa na la baadae. Mzazi usichukie pia pale mwanao atakapoonywa ama kuadhibiwa kwa makosa aliyofanya. Cha muhimu adhabu isiwe ndiyo kitu cha kukimbilia mtoto anapokosea, mpe elimu kwanza na akikaidi basi adhabu inayolingana kosa alilotenda itolewe. Usimlee kama yai,mlee kama mtoto. Kina baba jukumu la kulea ni la wazazi wote, baba na mama.
Mzazi, mlezi,ndugu jamaa, jamaa, marafiki na jamii kwa ujumla ni jukumu letu sote kulea na tunapaswa kulaumiwa sisi kwa tabia mbaya watakazokuwa nazo watoto waliopo katika jamii zetu.

Ni mategemeo yangu kwamba kwa pamoja tutajenga jamii imara na kuopata raia bora wa leo na hata kesho. Acha alama bora kwa mwanao ambayo kamwe haitafutika na atairithisha kwa wajukuu zako na hata kizazi chako chote.

Nina mengi ya kuandika lakini niishie hapa kwa leo. Tukutane katika makala zijazo, siku njema!.

Nickson Yohanes
nmyohanes@gmail.com
07538430303/ 0712843030