Hii ndiyo siri ya kuweza kupokea au kupata kitu chochote

Habari za leo ndugu msomaji wa mtandao huu wa PAMBAZUKA DAIMA ni matumaini yangu kwamba bado unaendelea kulisukuma gurudumu la maendeleo kwa kufanya kitu bora zaidi ya ulivyofanya jana.

Ndugu msomaji kuna siri katika kila kitu ambacho ukifanikiwa kuijua basi utaweza kufanikiwa katika eneo husika. Kuna siri za kufaulu mitihani shuleni, kuna siri za kuwa na familia bora na kadhalika. Naita siri lakini kiukweli sio siri kwani ni vitu ambavyo tunavijua ama tunaona kwamba havina maana katika maisha yetu na hivyo kutotilia maanani.

Labda nianze kwa kukuuliza swali hili; Ikiwa una ndoo ya maji iliyojaa maji tayari, ukitaka kuweka kitu kingine katika ile ndoo au maji mengine utafanyaje? Majibu yanaweza kuwa mengi lakini jibu la muhimu ni kuyatoa yale maji kwa kumwaga ama kumpa anaehitaji ili upate nafasi ya kuweka kitu kingine. Lakini litakuwa sio jambo jema kumwaga maji wakati kuna anaehitaji. Kwa hiyo basi siri ya kupokea kitu chochote ni kutoa, ndio kutoa kwa anaehitaji ili nawe upate nafasi ya kupokea kitu kipya. Kama hutatoa na wewe umeshajaza vitu katika sehemu yako ni dhahiri kwamba hakutakuwa na nafasi ya kupokea kitu kipya. Ndio maana tunashauriwa kutoa ili nasi tupokee, huwezi kuwa mtu wa kupokea pekee.


Tunapozungumza suala la utoaji tunamaanisha kitu chochote ambacho kinaweza kuwa msaada kwa mtu mwingine. Suala la kutoa sio lazima uombwe, ni muhimu zaidi kama ukitoa bila msukumo kutoka nje. Kitabu cha biblia kinawaasa watu kuwa kutoa ni bora kuliko kupokea na pia utapokea kadiri nawe unavyotoa, tena maradufu. Unapozungumzia suala la kutoa watu wengi hupeleka akili zao katika pesa. Kutoa pesa ni muhimu pia, lakini je kama huna pesa huna sifa ya kutoa? Unaweza kutoa kitu chochote kwa mtu yeyote ilimradi kina msaada kwake. Unaweza kutoa msaada, kutoa elimu, kusaidia wasiojiweza, kufundisha wenzako, kutoa muda wako kwa kusaidia wengine ama kuwatembelea wagonjwa, yatima na wale wanaohitaji faraja na hata kutoa sehemu ya mali zako kwa wengine. Kuna siri kubwa katika utoaji, ni siri ambayo haiwezi kuelezeka kirahisi ni siri kubwa sana ya kupokea chochote. Ila muhimu sana ni kwamba unapotoa kitu usitoe ukingoja shukrani au ukitegemea malipo kwani malipo yake utapata katika muda usioutegemea tena kwa mtu usiyemtegemea. Kuna msemo wa Kiswahili usemao ‘’Tenda wema nenda zako, usingoje shukurani’’.
Soma: Je umepanda nini shambani kwako?

Ndugu yangu unaesoma hapa nawe una kitu cha kutoa kwa watu wengine, usiwe mtu wa kupokea pekee bila kutoa. Kutoa hakukufanyi kufilisika bali kuendelea kuneemeka. Kama kutoa kungekuwa kunafilisi basi bilionea tajiri namba moja duniani Bill Gates angeshafilisika kitambo kwa misaada  anayotoa duniani kupitia mfuko wake wa Bill and Melinda Gates unaohusika kutoa misaada kwa watu masikini kote duniani. Kwa hapa nyumbani Tanzania basi mzee Reginald Mengi angekuwa ameshafilisika kitambo pia maana toka nilivyoanza kumsikia anatoa misaada kwa kweli angekuwa ameshaishiwa. Bilionea namba tatu kwa sasa ambae pia alishakuwa namba moja na mbili katika kipindi cha nyuma Warren Buffet nae ni mtoaji mzuri na amedhamiria kutoa 99%  ya utajiri wake kama misaada katika maisha yake yote. Hii ni tofauti kabisa na dhana hasi iliyojengekwa kwamba watu matajiri ni wabinafsi na wachoyo, jambo ambalo si kweli. Matajiri hupenda kusaidia hasa wale wanaonyesha nia ya kufanya jambo fulani zuri.

Kama wewe ni mwanafunzi na unalijua vizuri somo fulani kuliko mtu mwingine yeyote darasani kwako ukiamua kulifundisha hilo somo kwa wengine, si tu kwamba utakuwa umewasaidia wengine kufaulu somo linalowapa shida bali pia nawe utaimarika katika hilo somo kwa kupokea changamoto na kupokea elimu mpya kutoka kwa wengine.Pia itakusaidia kukumbuka kirahisi na kuonekana bingwa wa somo husika. Utafungua mlango wa wenzako kukusaidia katika masomo mengine ambayo wanayaweza vizuri kuliko wewe. Kinyume chake ni kwamba hutaona mafanikio mazuri katika masomo yako kama utakuwa mbinafsi. Kila mtu anaweza kutoa kitu, hata kama ni kidogo kiasi gani. Ndio maana hata katika dini zetu tunasisitiziwa kutoa zaka katika nyumba za ibada kama shukurani kwa Mungu wetu kwa aliyotujalia kupata.

Inaweza kukuwia vigumu pale unapoanza lakin utaweza kuzoea tabia hiyo ya utoaji kadiri unavyotoa kila mara. Unaweza kuanza kidogo kidogo mpaka pale utakapoona kwamba sasa huoni ugumu katika kutoa. Labda nikupe hadithi ya kweli; Mwaka fulani nikiwa sekondari, tulitoka shule mchana kama ilivyo ada. Tukitembea watatu njiani kuelekea nyumbani mmoja wetu (si mimi) alitoa kiasi fulani cha pesa kwa mlemavu aliekuwa anaomba barabarani, hatua kama tano mbele aliokota mara tano ya pesa aliyotoa kwa yule mlemavu. Unaona katika mfano huu jinsi kutoa kunavyofungua milango mingine, milango ya kupokea. Sikuambii kwamba ukitoa nawe utaokota hela kama rafiki yagu,hapana. Toa kwa kuwa umeguswa na ukiamini kwamba unawasaidia wengine kwa kile ambacho umejaaliwa kuwa nacho. Tahadhari tu kwa upande wa fedha uweze kutofautisha kati ya kutoa kusaidia na kutapanya pesa zako ovyo. Unaweza kuanza kwa kutenga asilimia ya mapato yako kwa kusaidia wengine. Muda wako nao ni wa thamani sana hivyo ni muhimu kuulinda na kutoutoa kwa wale wasiostahili.

Usisahau kupenda ukurasa wetu wa facebook kwa kubonyeza Pambazuka Daima Blog na pia kujiunga na orodha yetu ya barua pepe kupata makala kila mara zitokapo.

Nickson Yohanes
nmyohanes@gmail.com

Related Posts